Tuesday, December 12, 2017

NI ALAMA GANI ZA MWILI WAKO ZITAKUFAHAMISHA OVULATION IMEWADIA?



Wadau wa Kona ya Afya, niliahidi kuendeleza mada yetu ya namna ya kuzijua siku za kushika mimba kwa kuzungumzia baadhi ya alama za mwili zinazosaidia kutambua ni wakati gani Ovulation imewadia. Alama hizo za Ovulation si ngumu kuzitambua, iwapo utafahamu unatafuta alama gani. Kuna baadhi ya alama za mwili zinazokutahadharisha kwamba Ovulation iko njiani, hivyo kuweza kukusaidia kupanga vyema muda wa kujamiiana kwa ajili ya kupata mamba. Alama nyinginezo zinakufahamisha kwamba Ovulation imewadia au imeshapita. Ingawa alama hizo ziko nyingi na nitazungumzia baadhi ya hizo, lakini usifikiri kwamba unatakiwa utumie zote, kwani kufanya hivyo kunaweza kukuchanganya.
Iwapo hutoona alama zozote za Ovulation au iwapo siku zako za mwezi hazina mpangilio maalum, ni bora umuone daktari ambaye atakusaidia zaidi.
Mabadiliko ya joto lako la Mwili
Tunaweza kusema kuwa Joto lako la mwili au (Body Basal Temperature) ndio alama maarufu inayotumiwa na wanawake wengi ili kufahamisha kwamba Ovulation imewadia pale wanapotaka kubeba mimba. Hii ni kwa sababu joto lako la mwili huongezeka kwa kiasi kidogo na huendelea kuongezeka baada ya Ovulation. Ongezeko hilo la joto husababishwa na homoni ya progesterone, ambayo huongezeka sana punde baada ya Ovulation. Kwa kujipima joto lako la mwili na kuandika chati ya mabadiliko hayo unaweza kufahamu ongezeko hilo la joto lako la mwili. Unahitajia kipimamoto kwa ajili ya kufanikisha suala hilo. Zipo pimajoto maalum kwa ajili hiyo lakini unaweza kutumia pimajoto ya kawaida pia. Hakikisha unapima joto la mwili wako asubuhi baada ya kuamka na uhakikishe huna homa, hukukosa usingizi, hukunywa pombe, si mgonjwa wala huna wasiwasi na fikra nyingi. Ni bora ufanye hivyo kwa mizunguko kadhaa ya siku zako ili uweze kuijua vyema chati ya mabadiliko ya joto la mwili kwa mujibu wa mzunguko wako wa mwezi. 



Ingawa njia hii haianishi moja kwa moja kuwa Ovulation imewadia, lakini joto la mwili huongezeka kidogo kabla yakipindi hicho na huongezeka kwa kwa degree 0.4 hadi 0.6 baada tu ya kumalizika Ovulation. Kuongezeka joto kwa kiasi kikubwa baada ya Ovulation huendelea hadi siku utakayopata siku zako ambapo hupungua na mzunguko wako wa mwezi huanza tena. Iwapo utakuwa umepata mimba joto lako la mwili litaendelea hivyo hivyo kuwa juu. Kwa kuwa mabadiliko ya joto hutokea wakati wa Ovulation iwapo unajaribu kubeba mimba, kufuatilia mabadiliko hayo kwa muda usiopungua miezi miwili ni jambo la dharura ili uweze kujua wakati wa Ovulation ambapo una uwezekano mkubwa wa kubeba mimba. 
Mabadiliko ya majimaji ya ukeni
Wakati Ovulation inakaribia majimaji ya ukeni hubadilika pia kwa kiasi na hali. Ikiwa hakuna Ovulation majimaji ya ukeni huwa yanayonata au kama kremu au hukosekana kabisa. Wakati Ovulation inakaribia majimaji ya ukeni huongezeka na huwa katika hali ya majimaji na wakati mwingine huwa rangi nyeupe kama ya yai bichi. Iwapo utapima kwa vidole vyako huvutika kwa inchi au zaidi kati ya vidole vyako.
Ni bora nikumbushe hapa kwamba, kuan wakati unaweza kuwa na majimaji ya ukeni yanayofanana na ya wakati wa Ovulation hali ya kuwa huko katika Ovulation. Hali hiyo ni ya kawaida kwa watu wenye PCOS. Kutumia dawa za Clomid au Antihistamin huweza kufanya majimaji ya ukeni yakauke na hivyo kuwa vigumu kutumia njia hii ili kujua ni zipi siku zennye uwezekano mkubwa wa mimba. Njia hii huhesabiwa kuwa yenye itibari zaidi. 
Ongezeko la Matamanio 
Inaonekana kuwa maumbile nayo hutusaidia kujua ni siku gani tunaweza kubeba mimba! Wataalamu wameonyesha (jambo ambalo pengine wengi wameshalihisi) kwamba wanawake wanapokuwa katika siku zenye uwezekano mkubwa wa kupata mimba, matamanio yao ya huongezeka. Hizo ni siku chache kabla ya kujiri Ovulation, ambapo ndio wakati unaofaa wa kujamiiana iwapo unataka kubeba mimba. 
Hata hivyo njia hii si ya kutumainiwa sana kwani baadhi ya hali kama vile msongamano wa mawazo, fikra nyingi na wasiwasi huweza kupunguzaa matamanio. Au mtu anaweza akahisi matamanio katika muda wote wa mzunguko wa mwezi. 
Mabadiliko ya Ukeni:
Kama ambavyo majimaji ya ukeni yanavyobadilika wakati wa Ovulation, uke nao (cervix) hubadilika wakati wa kukaribia Ovulation. Wakati huo uke husogea mbele, huwa laini na hufunguka zaidi. 
Maumivu kidogo katika Matiti:
Baadhi ya wanawake wakati wanapokaribia Ovulation au baada ya hapo matiti yao huwa na maumivu kidogo. Suala hili huhusiana na mabadiliko ya homini mwili ambazo hujitayarisha kwa ajili ya mimba. Hata hivyo njia hii sio yenye kutegemewa sana kwani maumivu ya matiti huweza kusababishwa na masuala mengine. Pia maumivu ya matiti hutokea kabla ya hedhi au baada ya kutumia baadhi ya dawa za kusaidia uzazi. 




Alama nyinginezo
Baadhi ya wanawake huhisi maumivu kidogo ya tumbo ambayo baadhi huyaita Middle Pain. Maumivu hayo kwa kawaida hutokea upande ule yai linapotoka yaani upande wa Ovulation. Maumivu hayo hutokana na mwendo wa yai wakati linapopenya kwenye mirija. Maumivu hayo si ya kuendelea na wala si makubwa na huisha haraka. Hali hiyo huweza kutokea mara kadhaa katika siku za Ovulation. Kuna baadhi ya alama kama vile baadhi ya wanawake huhisi kichefuchefu, gesi, kukojoa mara kwa mara na maumivu wakati wa kujamiina, hali ambayo haitokei kwa watu wengi. Pia kuna baadhi ya vifaa vinavyopaatikana katika madula ya dawa katika baadhi ya nchi ambavyo huweza kukusaidia kujua wakati wako wa Ovuation umewajia, vifaa hivyo hujulikana kama 'Ovulation Kit"
La muhimu ni kufahamu kuwa wanawake hutofautiana katika kupata alama hizi, kwani kuna baadhi wanaweza wakapata baadhi ya alama hizi na wengineo wakapata nyinginezo. Kuuelewa vyema mwili wako ni jambo zuri linaloweza kukusaidia kuzijua siku zako la Ovulation na hivyo kuweza kujua siku zako za kubeba mimba